Wednesday 24 June 2015

Fadhila za kumsalia Mtume saw

Imeandikwa na alhidaaya.com

Allaah سبحانه وتعالى Anasema,

((إِنَّ اللَّهَ وَمَلَائِكَتَهُ يُصَلُّونَ عَلَى النَّبِيِّ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا صَلُّوا عَلَيْهِ وَسَلِّمُوا تَسْلِيمًا))

((Hakika Allaah Anamteremshia Rehma Mtume; na Malaika Wake (wanamuombea du'aa kwa vitendo vizuri alivyovifanya), Enyi mlioamini! Mswalieni (Mtume - muombeeni Rehma) na muombeeni amani)) [ Al-Ahzaab:56]

 

 

Hii ni amri kutoka kwa Allaah سبحانه وتعالى tumswalie Mtume صلى الله عليه وآله وسلم na juu ya hivyo kuna fadhila kubwa kumswalia kwake kamailivyothibiti katika Hadiythi nyingi zifuatazo:

 عنْ عبد اللَّه بن عمرو بن العاص ، رضي اللَّه عنْهُمَا أنَّهُ سمِع رسُول اللَّه صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم يقُولُ : ((من صلَّى عليَّ صلاَةً ، صلَّى اللَّه علَيّهِ بِهَا عشْراً))   رواهُ مسلم

Imetoka kwa 'Abdullaah bin 'Amru bin Al'-Aasw رضي اللَّه عنْهُمَا kwamba kamsikia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم anasema, ((Atakayeniswalia (atakayeniombea) mara moja Allaah Atamswalia (Atampa rahma) mara kumi)) [Muslim]

Subhaana Allaah! Hii ni fadhila tukufu kabisa kwamba Mola Aliyetuumba Atuswalie sisi waja wake mara kumi tutakapomswalia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم mara moja tu! Ukipima utaona fadhila hii haimkalifu mtu zaidi ya dakika moja!

 

Maana ya Swalah ya Allaah سبحانه وتعالى na Malaika Wake

Swalah ya Allaah سبحانه وتعالى  kwa waja Wake ni: Rahma na kuwasifu kwa Malaika.

Swalah ya Malaika kwa Waumini  ni: du'aa na kuwaombea Maghfirah.

عن ابن مسْعُودٍ رضي اللَّه عنْهُ أنَّ رسُول اللَّهِ صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم قال : (( أَوْلى النَّاسِ بي يوْمَ الْقِيامةِ أَكْثَرُهُم عَليَّ صلاةً)) رواه الترمذي وقال : حديثٌ حسنٌ

Imetoka kwa ibn Mas'uud رضي اللَّه عنْهُkwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلمamesema,

((Watu wa mwanzo kwangu (watakaokuwa karibu yangu) siku ya Qiyaamah ni wale wanaoniswaliasana))  [At-Tirmidhy na kasema ni Hadiythi Hasan]

 

Fadhila nyingine hii ya kuwa karibu kabisa na Mtume  wetu mpenzi  صلى الله عليه وآله وسلم. Nani asiyetaka kuwa na karibu naye siku ya Qiyaamah?

 عن أوس بن أوس ، رضي اللَّه عنْهُ قال : قالَ رسولُ اللَّه صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم : (( إنَّ مِن أَفْضلِ أيَّامِكُمْ يَوْمَ الجُمُعةِ ، فَأَكْثِرُوا عليَّ مِنَ الصلاةِ فيه ، فإنَّ صَلاتَكُمْ معْرُوضَةٌ علَيَّ)) فقالوا : يا رسول اللَّه ، وكَيْفَ تُعرضُ صلاتُنَا عليْكَ وقدْ أرَمْتَ ؟ ، يقولُ : بَلِيتَ ، قالَ: (( إنَّ اللَّه حَرم على الأرْضِ أجْساد الأنْبِياءِ )) . رواهُ أبو داود بإسنادٍ صحيحِ

Imetoka kwa Aws ibn Aws   رضي اللَّه عنْهُ kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema ((Siku iliyo bora kabisa kwenu ni siku ya Ijumaa, kwa hiyo zidisheni kuniswalia (siku hiyo) kwani Swalah zenu zinaonyeshwa kwangu)) Wakasema (Maswahaba) Ewe Mjume wa Allaah vipi Swalah zetu zinaonyeshwa kwako na hali utakuwa umeoza?  Akasema, ((Allaah Ameharamisha ardhi kuila miili ya Mitume)) [Abu Daawuud kwa isnaad ya Sahiyh]

 عنْ أبي هُريْرةَ رضي اللَّه عنهُ قال : قال رسُولُ اللَّه صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم : (( رَغِم أنْفُ رجُلٍ ذُكِرْتُ عِنْدَهُ فَلَمْ يُصَلِّ علَيَّ))  رواهُ الترمذي وقالَ : حديثٌ حسنٌ .

 

Imetoka kwa Abu Hurayrah رضي اللَّهkwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلمamesema, ((Amepata khasara mtu ambaye nimetajwa kwake na hakuniswalia)) [At-Tirmidhiy na kasema Hadiyth Hasan]

 عنْ أبي هُريْرةَ رضي اللَّه عنهُ أنَّ رسُولَ اللَّه صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم قال : (( ما مِنْ أحد يُسلِّمُ علَيَّ إلاَّ ردَّ اللَّه علَيَّ رُوحي حَتَّى أرُدَّ عَليهِ السَّلامَ )) . رواهُ أبو داود بإسناد صحيحٍ

Imetoka kwa Abu Hurayrah رضي اللَّهkwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلمamesema,

((Yeyote atakayeniswalia hurudishiwa roho yangu hadi nimrudishie salaam))[Abu Daawuud kwa isnaad ya Hasan]

 

Ni jambo la ajabu kwetu kuwa roho yake Mtume صلى الله عليه وآله وسلمhurudishiwa kwa ajili ya kujibu salaam zetu tu.

 وعن علِيٍّ رضي اللَّه عنْهُ قال : قال رسُولُ اللَّهِ صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم : (( الْبخِيلُ من ذُكِرْتُ عِنْدَهُ ، فَلَم يُصَلِّ علَيَّ )) رواهُ الترمذي وقالَ : حديثٌ حسنٌ صحيحٌ .

Imetoka kwa 'Aliy رضي اللَّه kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلمamesema, ((Bakhili ni yule ambaye nimetajwa kwake na hakuniswalia))[At-Tirmidhiy na kasema ni Hadiyth Hasan Swahiyh]

 

Bila shaka hakuna anayependa kuwa na sifa hiyo, na sio ubakhili wenye uhusiano na  fedha bali ni kwa kutokumswalia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم.

 

Vipi kumswalia Mtume?صلى الله عليه وآله وسلم

 عنْ أبي مسْعُود الْبدْريِّ ، رضي اللَّه عنْهُ ، قالَ : أَتاناَ رسُولُ اللَّهِ صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم ، وَنَحْنُ في مَجْلِس سعد بنِ عُبَادَةَ رضي اللَّه عنهُ ، فقالَ لهُ بَشِيرُ بْنُ سعدٍ : أمرَنَا اللَّه أنْ نُصلِّي علَيْكَ يا رسولَ اللَّهِ ، فَكَيْفَ نُصَّلي علَيْكَ ؟ فَسكَتَ رسولُ اللَّه صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم ، حتى تَمنَّيْنَا أنَّه لمْ يَسْأَلْهُ ، ثمَّ قال رسولُ اللَّه صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم  (( قولُوا : اللَّهمَّ صلِّ عَلى مُحَمَّدٍ ، وَعَلى آلِ مُحمَّدٍ ، كما صليْتَ على آل إبْراهِيم ، وَبارِكْ عَلى مُحَمَّد ، وعَلى آلِ مُحمَّد ، كما بَاركْتَ عَلى آل إبْراهِيم ، إنكَ حمِيدٌ مجِيدٌ ، والسلام كما قد عَلِمتم ))رواهُ مسلمٌ

Imetoka kwa Abu Mas'uud Al-Badriyرضي اللَّه عنْهُ ambaye amesema, alitujia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم na sisi tulikuwa katika majlis (ukumbi) wa Sa'ad ibn 'Ubaadah رضي اللَّه عنْهُ Bashiyr ibn Sa'ad akamwambia, Allaah Ametuamrisha tukuswalie ewe Mjumbe wa Allaah, je, Vipi tukuswalie? Akanyamaza Mtume صلى الله عليه وآله وسلم mpaka tukatamani kwamba asingelimuuliza. Kisha akasema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم((semeni: Allaahumma Swalli 'Alaa Muhammadin Wa 'alaa aali Muhammadin Kamaa Swallayta 'alaa aali Ibraahiym, Wa Baarik 'alaa Muhammadin Wa 'alaa aali Muhammadin Kama Baarakta 'alaa aali Ibraahiym Innaka Hamiydum-Majiyd. Na salaam kamamlivyofundishwa)) [Muslim]

 

Basi ndugu Waislamu tusiziache fadhila tukufu na nyingi kama hizo kwa kumswalia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kila mara, ndimi zetu ziwe daima zikimswalia na kufanya hivyo pia  inaingia katika fadhila za kumkumbuka Allaah سبحانه وتعالى. 

 

Allaahumma Turuzuku mapenzi Yako na mapenzi ya Mtume صلى الله عليه وآله وسلم na Tujaaliye tuwe karibu yake katika Pepo ya Firdaws.  Allaahumma  Mpe Mtume Muhammad صلى الله عليه وسلم)  wasila, na fadhila, na Mfikishe daraja yenye kusifiwa, ambayo Umemuahidi.

 

Sunday 24 May 2015

MWEZI WA SHAABAN NA FADHILA ZAKE

Imeandaliwa na Raudhwah group

Mwezi wa Shaaban ni mwezi wa nane katika miezi ya kiislamu. Mwezi huu upo kati ya Rajab na Ramadhan. Rajab na Ramadhan ni katika miezi mitukufu. Ni mwezi ambao Muislamu anatakiwa ajihimu katika kufanya ibada. Pia ni mwezi ambao mja autumie katika kujiandaa zaidi na Ramadhan ili asiweze kupoteza fursa ya Ramadhan ikiwa Allah atamjaalia kufika. Pia husemwa kuwa umeitwa kwa jina la Shaaban kwa sababu ya waaarabu kutawanyika kwao katika kutafuta maji au katika mashambulizi baada ya kutoka mwezi wa Rajab. 

Miongoni mwa mambo ambayo yamependekezwa sana mja ayafanye ndani ya mwezi wa Shaaban ni kufunga. Kabla ya kuangalia ubora wa funga ndani ya Shaaban na vipi imethibiti, kwanza tuangalie umuhimu wa mja kufunga siku tu kwa ajili ya Allah. 

Imepokewa na Abi Said Al Khudri (Radhi za Allah ziwe ju yake) amesema: “Amesema Mtume wa Allah "Hakuna mtu yoyote anayefunga siku yeyote katika njia ya Allah Mtukufu isipokuwa Allah huuweka mbali uso wake na moto kwa siku hiyo aliyofunga miaka sabiini ". Imepokelewa na Bukhari na Muslim. Pia imepokewa na Amri Ibn Abass (Radhi za Allah ziwe juu yake) amesema: Amesema Mjumbe wa Allah (swalla Allahu alayhi wasallam) "Mwenye kufunga siku yeyote katika njia ya Allah moto huwa mbali naye kwa mwendo wa miaka mia moja”.Imepokelewa na Attbraniy

Hadithi tulizozitaja hapo juu zinaonesha wazi uzito wa mja kufunga siku moja tu kwa ajili ya Allah (subhanahu wata‘ala). Hivyo ndugu yangu Muislamu usiwe mzito kwa kusema hizi funga za sunna tu. Kimbilia funga za sunna ili uweze kupata kheri kama hizo. Na zifunge saumu zako kwa kutaraji malipo kutoka kwa Allah (subhanahu wata‘ala).

KUPENDEKEZWA KUFUNGA KATIKA MWEZI WA SHAABAN NA FADHILA YA FUNGA HIYO

Kutoka kwa Bibi Aysha (radhi za Allah ziwe juu yake) amesema: “Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa akifunga hadi tukadhani kuwa hatofungua kamwe, na alikuwa akiacha kufunga hadi tukadhani hatofunga tena. Sijamuona Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) kufunga mwezi mzima kama alivyokuwa akifunga Ramadhaan, na sijamuona akifunga mara nyingi kama alivyofunga katika Shaabaan” Bukhaari na Muslim.

Kwa hakika Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa akikithirisha zaidi kufunga ndani ya mwezi wa Shaaban kuliko miezi mengine yoyote ukitoa mwezi wa Ramadhan. Na katika hili Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) mwenyewe alieleza ni kwa nini hufunga zaidi ndani ya mwezi wa Shaaban. Imepokewa kutoka kwa Usama Ibn Zaid (Radhi za Allah ziwe juu yake) amesema: Nilisema ewe Mjumbe wa Allah sikukuona ukifunga katika mwezi wowote katika miezi kama siku unazofunga katika mwezi wa Shaaban? Akasema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) Huo ni mwezi ambao watu wameghaflika nao baina ya Rajab na Ramadhan nao ni mwezi ambao (hurufaishwa) hupandishwa ndani yake amali za watu kwa Bwana wa Viumbe na napenda zipandishwe amali zangu na hali ni mwenye kufunga.” Imepokelewa na An-nasai.

Huyu ni kipenzi cha Allah ambae amesamehewa dhambi zake zilizopita na zinazokuja ila alikuwa akijihimu kwa kufunga ili a’amali zake zipelekwe kwa Allah hali ya kuwa amefunga. Je vipi mimi na wewe ambao daima ni wenye kumkosea Allah? Kwa nini na sisi tusijikurubishe kwa Allah kwa kufunga sana ndani ya mwezi wa Shaaban? Isitupite fursa hiyo na tujihimize katika suala zima la kufunga sisi wenyewe pamoja na watu wetu.

JE MTU AKITAKA KUFUNGA MWEZI MZIMA WA SHAABAN INASIHI?

Katika kauli yenye nguvu zaidi wanazuoni wanasema kuwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) hakuwahi kufunga mwezi wowote kamili ambao ni sunna kufunga. Na hili linatokana na ushahidi kuwa imepokewa kutoka kwa Ibn Abbas (radhi za Allah ziwe juu yake ) amesema "‘‘Mtume wa Allaah (swalla Allahu alayhi wasallam) hakuwahi kufunga mwezi wowote kikamilifu isipokuwa Ramadhan." (Bukhaari).

MLANGO WA KUKATAZWA KUFUNGA NUSU YA MWISHO YA SHAABAN

Imekatazwa kufunga katika mwisho wa Shaban kwa nia ya kutozikosa siku za mwanzo wa Ramadhani. Na hili linathbitishwa kuwa imeripotiwa katika Sahihi Bukhari kutoka kwa Abu Hurayrah (radhi za Allah ziwe juu yake) kuwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema: “Kufunga katika mwisho wa Shaaban kumekatazwa ili kuweka tofauti kati ya funga za Sunna na funga za faradhi.”

TANBIHI

Wale wenye tabia na mpangilio wa kufunga na ikawa siku za mwisho za Shaaban zimetokezea sambamba na siku ambazo mtu yule kawaida huwa anafunga, kama vile za Jumatatu na Alhamis, au funga ya Nabii Daud au imemkuta akiwa anaendelea kulipa saum ya deni basi hawa wao wanaruhusika kufunga.

MLANGO WA KUKATAZWA KUITANGULIA RAMADHANI KWA SAUMU YA SIKU MOJA AU MBILI

Imepokewa kutoka kwa Abu Huraira (Radhi za Allah ziwe juu yake) kutoka kwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema : “Asiitangulie mmoja wenu Ramadhani kwa saumu ya siku moja au mbili isipokuwa akiwa mtu alikuwa akifunga saumu yake basi na aifunge siku hiyo” Bukhari na Muslim.

Amesema Tirmidhi (3/69) na wanavyuoni wanaitumia hadithi hii, kwa kuchukia mtu kufanya haraka kufunga kabla kuingia mwezi wa Ramadhani. Ila mwenye kuzoea kufunga siku za jumatatu na alhamisi au siku tatu za kila mwezi au saumu ya Nabii Daud, ikawafiki saumu yake siku hiyo basi na afunge kama kawaida yake kwa sababu makatazo hayamuelekei yeye, kinyume cha mwenye kuanzia kufunga hali ya kuwa si wajibu kwake na wala hatakiwi kulipa wala si ada kwake, haitakiwi kwake kufunga.
Pia Yaumu Shakka kumekatazwa mtu kufunga. Yawmu Shakk (siku yenye shaka) ni ile siku ambayo watu hawana uhakika juu ya kuanza kwa Ramadhan, kwa sababu ya hali ya mawingu kufunga na mwezi kutoonekana au sababu nyinginezo.

Imepokewa kutoka kwa Swila Ibn Zufar “Tulikuwa kwa Ammar Ibn Yaser akaletewa mbuzi wa kuchoma akasema" Kuleni " akakaa mbali mmoja katika watu akasema “Hakika mimi ni mwenye kufunga” akasema Ammar “mwenye kufunga siku ambayo watu huitilia shaka basi amemuasi Abal Qassim (swalla Allahu alayhi wasallam). Bukhari.

Pia Muislamu anatakiwa ajihimu katika kufanya mambo mengine mbali mbali ya kheri kama kuswali swala za sunna, kuleta istighfaar na adhkaaar nyenginezo kwa wingi, kutoa sadaka kwa wingi na kheri nyengine. Haya yote mwenye kuyafanya yatamuandaa katika kuitumia Ramadhani yake vile ipasavyo.

UKUMBUSHO 

Wale wote wenye madeni ya swaumu, basi wasiwache kulipa madeni yao. Kwani hairuhusiwi mtu kuchelewesha kulipa deni la Ramadhani hadi ikaingia Ramadhani nyengine. Na mtu anaweza kuzilipa funga hizo ndani ya Shaaban kwa ushahidi kutoka kwa Mama wa Waumini Aysha (radhi za Allah ziwe juu yake) amesema : “Ilikuwa ninazo siku za kulipa za Ramadhaan na sikuweza kuzilipa isipokuwa (katika mwezi wa) Shaaban.” Bukhaari.

Yeyote aliyekuwa na uwezo wa kulipa Swawm zilizompita kabla ya Ramadhaan (ya pili) kuingia na asifanye hivyo, basi atalazimika kuzilipa baada ya Ramadhaan (ya pili), pia analazimika kutubia na kumlisha maskini mmoja kwa kila siku iliyompita. Huu ni msimamo wa Imam Maalik, Ash-Shafi’iy na Ahmad.

Na Allah ni mjuzi zaidi.

Tuesday 7 April 2015

Umoja wetu ni nguvu yetu


Kimsingi maana ya umoja na mshikamano kati ya Waislamu si kuwataka wafuasi wa madhehebu mbalimbali za Kiislamu kutupilia mbali itikadi zao, bali lengo kuu ni kujenga maelewano na mshikamano mbele ya adui wao wa pamoja. Naam, tofauti hizo za kimadhehebu zinaweza kujadiliwa kwa njia za kimantiki na busara katika vikao vya mijadala ya kielimu vya wanazuoni na maulamaa wa Kiislamu na kufikia nukta za wazi. Hapana shaka kuwa makelele na malumbano yasiyokuwa ya kielimu katika vikao vya umma kuhusu masuala ya kitaalamu hayawezi kuwa na matunda ya kuridhisha. Tunaweza kusema hapa kuwa moja ya vizuizi vya umoja na mshikamano katika umma ni kutolewa mijadala kama hiyo ya kielimu na kitaalamu kuhusu masuala ambao Waislamu wanatofautiana juu yake katika vikao vya umma na kwa njia ya kichochezi.
Dini tukufu ya Kiislamu inawalingania wafuasi wake wote kutumia akili na kutafakari na kuzidisha maarifa na elimu yao kadiri inavyowezekana. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, kuwa na maarifa na elimu huzuia mifarakano na ukosefu wa maelewano. Inasikitisha kuona kwamba katika zama za sasa za mawqasiliano na utandawazi Waislamu wa madhehebu moja hawajui kabisa au wana maarifa finyu kuhusu itikadi za ndugu zao wa madhehebu nyingine ya Kiislamu. Upungufu huu wa maarifa kuhusu itikadi za madhehebu tofauti za Kiislamu umekuwa moja ya vizuizi vya umoja na mshikamano wa Kiislamu na umekuwa ukisababisha mambo mengi ya kusikitisha katika ulimwengu wa Kiislamu.
Mwanafikra mmoja wa Kiislamu anasema: "Tishio linalowakabili Waislamu kutokana na hali ya kutofahamiana na kudhaniana vibaya ni kubwa zaidi kuliko lile linalotokana na tofauti zao za kimadhehebu."
Mwingine anasema kuhusu taathira mbaya za kutofahamiana kati ya Waislamu na mchango wake katika kukuza hitilafu kwamba: "Tofauti za kimadhehebu na kiitikadi ni jambo ambalo limekuwepo katika zama zote lakini jambo linalobadilika kila wakati na katika kila zama ni ukosefu wa maelewano na kutofahamiana kwa pande husika. Kwa sababu hiyo, moto wa ugomvi, malumbano na mifarakano huchochewa zaidi na zaidi."
Sheikh Muhammad Abu Zahra ambaye alikuwa miongoni mwa maulamaa wa chuo cha al Azhar cha Misri amesema:
"Tofauti na hitilafu zilizoko kati ya Waislamu zimepenya na kuingia zaidi katika fikra, hisia na nyoyo zao kutokana na taasubi na chuki za kikaumu na kimadhehebu kwa kadiri kwamba Muislamu mmoja humuangalia Muislamu mwenzake anayehitilafiana naye kifikra kama adui aliyeko mafichoni dhidi yake na si kama mtu mwenye mitazamo tofauti kama yeye anayefanya jitihada za kujua hakika ya sheria za Mwenyezi Mungu."

Amkeni wapendwa waislamu
umoja wetu ni nguvu yetu
Imeandikwa na Sheikh Rashid Ashukery.

Friday 26 December 2014

SHEMEJI NA MIPAKA YAKE YA KISHERIA NDANI YA UISLAMU


Kila sifa njema zinamstahikia Allah (subhanahu wa ta‘ala) Muumba wa kila kilichomo katika ulimwengu huu. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam).

Shemeji huwa ni ndugu wa kiume wa mume kwa mke au ni ndugu wa mke kwa mume. Watu hutumia neno shemeji katika kuonesha uhusiano uliokuwepo baina yao. Lakini leo hebu tuangalie ni yapi yanayofanywa ndani ya jamii za kiislamu baina watu na shemeji zao na uharamu wake ndani ya uislamu.

Kwanza tambua ewe ndugu yangu mpenzi kuwa shemeji yako si mahaarim yako(anaweza kukuoa au unaweza kumuoa). Wako watu hudhani kuwa shemeji yake hana neno. Hayo ni makosa lazima sheria za kiislamu zichungwe wakati wa kukaa nae.

Amesema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam)“Tahadharini na kuingia kwa wanawake(kuingia majumbani mwao)”. Akaulizwa: “Je, ndugu wa mume [shemeji])”. Akasema (Swalla Allahu alayhi wasallam): “Huyo (shemeji) ni mauti” (Bukhari na Muslim).

Miongoni mwa mambo yasiyofaa kufanywa mbele ya shemeji na jamii zetu wanajisahau nayo:

1-Kutovaa hijabu ya kisheria. Wako baadhi ya waislamu wanadhani kuwa mbele ya shemeji yake anaweza kuvaa vyovyote. Kwa mfano mwanamme unamkuta amevaa bukta haisitiri magoti au amekaa tumbo wazi mbele ya mke wa kaka yake. Au mwanamke kuvaa nguo za kubana au kutembea bila ya stara kichwani au vazi lolote lile analovaa ndani. Hayo yote ni makosa na hayafai ndani ya uislamu.

Tena la kusikitisha waume au wake wamekaa kimya wakidhani na wao ni sahihi au wanajua ovu bali wananyamaza. Na hili ni miongoni mwa sababu zinazopeleka kusikia kesi amemchukua mke wa kaka yake au mume wa dada yake. Ndio inachangia mume au mke anaona umbo la shemeji yake. Unadhani nini kitatokea?

Anasema Allah (subhanahu wataala) “Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao isipo kuwa unao dhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao, au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au kaka zao, au wana wa kaka zao, au wana wa dada zao, au wanawake wenzao, au iliyo wamiliki mikono yao ya kuume, au wafwasi wanaume wasio na matamanio, au watoto ambao hawajajua mambo yaliyo khusu uke. Wala wasipige chini miguu yao ili yajuulikane mapambo waliyo yaficha. Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa.”(Suratu Nnur : 31).

Aya iko wazi hapo kuwa shemeji hajatajwa. Kwa nini waislamu tuige mila za mayahudi na manasara?
Pia imekatazwa kujipamba mbele ya shemeji. Kama tulivyosema yeye si maharimu yako hivyo hatakiwi akuone unapojipamba au ulivyojipamba. Ila hili ni msiba kwa wanawake wa sasa maana wanajipamba na wanaranda majiani waonekane na kila mwanamme.

2- Kukaa faragha au kutoka pamoja faragha. Shemeji si maharim yako. Hivyo haipaswi mukae faragha baina yenu. Ila jamii ilivyojisahau unamkuta mtu anarudi harusini usiku anaenda kuchukuliwa na shemeji yake. Wako peke yao wanarudi. Mtu na shemeji yake wanatoka peke yao bila ya maharim baina yao wanakwenda safari zao na kurudi. Haya nayo ni makosa. Na mume au mke ndio wa kwanza kusema mpeleke shemeji yako safari zake.

Kwa nini makosa? Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) anasema: “Mwenye kumuamini Allah na siku ya mwisho, basi asikae peke yake na mwanamke asiyekuwa maharimu yake pamoja naye, kwani watatu wao ni shetani” (Ahmad).

Mtume (Swalla Allahu alayhi wasallam) amesema: "Hawi faraagha mmoja wenu pamoja na mwanamke ila awepo Mahram wake" (Bukhari Na Muslim)

Hadithi zinaonesha moja kwa moja kuwa haya yenye kufanywa hayafai. Shemeji si maharim yako. Bora jamii ikuone tofauti kwa kufuata sheria za Allah (subhanahu wataala) kuliko kuwaridhisha wao na unamkera Allah (subhanahu wataala).

3-Miongoni mwa makosa mengine yanayofanywa ni kwa kupeana mikono wakati wa kusalimiana au waki zungumza, Amesema Mjumbe wa Allaah (Swalla Allahu ‘alayhi wasallam): “Mmoja wenu kuchomwa [kudungwa] katika kichwa chake (na katika Riwaya: (cha mwanamme) kwa msumari au sindano ya chuma ni bora kwake kuliko kumgusa mwanamke asiyekuwa halali kwake.” Imepokelewa na Atw-Twabaraaniy.

Mtu na shemeji yake wanapiga picha huku wameshikana mikono au kamkumbatia shemeji yake. Au mwanamke anapiga picha na shemeji yake wakati mwanamke amevaa vazi lisilo la kisheria. Wenyewe wanasema wanaishi kizungu. Ila tambua hayo yote ni makosa. Na haitakikani waislamu tuchukue mila za mayahudi na manaswara tujipambe nazo. Ni lazima tujiepushe nazo.Maana mambo haya yanafanywa na wasiokuwa waislamu na muislamu anafanya ili na yeye aonekane anaenda na wakati. Ila atambue yamekatazwa katika uislamu.

Na wala hatusemi mtu asizungumze na shemeji yake. Wazungumze wakae vizuri ila iwe chini ya muongozo uliowekwa na dini yetu. Na kufuata sheria za kiislamu ni kujenga heshima baina yenu na udugu uliokuwa bora. Utakaoepusha fitna na ugomvi baina ya ndugu na familia.

Na tambua ewe muislamu, uislamu haukuweka haya ila kwa maslahi. Kesi za shemeji zimezidi sana ndani ya jamii zetu. Tatizo sisi tuko mbali na maamrisho ya dini zetu na tumekumbatia mila za kikafiri. Nafsi ya mtu usiibebee dhamana.Kwani nafsi daima inaamrisha maovu. Allah (subhanahu wataala) anasema “Kwa hakika nafsi ni mno kuamrisha maovu “ (Suratu Yuusuf : 53). Na huwezi kujua ni mbinu gani anazoweza kutumia sheytwan.

Ishi katika njia ya Allah ili upate furaha hapa duniani na kesho akhera.

Thursday 18 December 2014

NASAHA MUHIMU SANA KWA WATUMIAJI WA SIMU ZA MIKONONI,FACEBOOK,WHATSAPP NA MITANDAO MENGINE YA KIJAMII


Anasema Allah (subhanahu wataala) “Na tukambainishia zote njia mbili“(Suratul Balad :10). na akasema tena “Hakika Sisi tumembainishia Njia. Ama ni mwenye kushukuru, au mwenye kukufuru.”(Suratul Insaan :3).

Aya mbili za juu zinaonesha ni vipi ambavyo Allah (subhanahu wataala) amempa uhuru wake mwanadamu. Allah (subhanahu wataala) amembainishia mwanadamu njia mbili. Na akamwambia njia hii ukiifuata basi utapata radhi zangu na ukiikataa njia hii ukafuata njia nyengine basi huko utapata ghadhabu zangu. Allah (subhanahu wataala) akamuacha mwanadamu achague mwenyewe ni wapi pakufuata. Na kumuacha huku si kwa lengo jengine ila ni kumpa mtihani. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Ambaye ameumba mauti na uhai ili kukujaribuni ni nani miongoni mwenu mwenye vitendo vizuri zaidi.” (Suratul Mulk :2).

Wengi wa wanaadamu wameghafilika na uhuru walopewa. Na hakuna kinachowaghafilisha ila ni pumzi za dunia na starehe zake. Badala ya kufuata njia ya kheri amekuwa akiifuata njia ya shari na akafanya matamanio yake ndio mola wake. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Je! Umemwona aliye fanya matamanio yake kuwa ndiye mungu wake”(Suratul Jaathiyah : 23).

Na mwanadamu huwa anajua kama amepewa uhuru huo. Kwani hata anapokumbushwa neno la Allah au kukatazwa usifanye hiki kibaya hujibu kaburi lako au langu? Pesa ninayoitoa yangu ya yako? Wewe inakuhusu nini? Yote hayo ni miongoni mwa majibu yake. Lakini kwa uwezo wa Allah tusichoke katika kuwakumbusha na kujikumbusha.

Sasa tuangalie uhuru wake mwanadamu na kipi ataenda kumjibu Allah (subhanahu wataala)?

1-Muislamu amepata simu kutoka njia yoyote ile iwe ya halali au ya haramu. Lengo la simu hiyo ni kwa ajili ya mawasiliano. Anajua mwenyewe yawe ya kheri au ya shari. Lakini hebu ajiulize yafuatayo : Mauti yakimfika na simu yake iko mkononi mwake au mfukoni mwake, Je Allah (subhanahu wataala) atakuwa radhi na yeye?

Ili Allah (subhanahu wataala) awe radhi nae maana yake kusikuwemo na lolote lile la haramu la kumkera Allah (subhanahu wataala).

Au Allah (subhanahu wataala) hatokuwa radhi nae kwa sababu ndani ya simu yake imejaa message za matusi,mapenzi na mazungumzo ya haramu? Au ndani ya simu yake imejaa namba za wanaume au wanawake ambao husema ni wapenzi wake wa haramu? Au ndani ya simu yake kuna video za ngono na nyimbo? Au yeye ameoa au ameolewa lakini hutumia simu yake kutoka nje ya ndoa? Au hutumia simu yake kuwadhulumu watu na kufanya mambo ya riba au kuiba?

Nini atamjibu mwanadamu huyu Allah (subhanahu wataala)? Je anajitengenezea njia gani kwa Allah? Hebu jiulize masuala haya sasa hivi ikiwa mtu atafikwa na mauti. Je simu yake inamridhisha Allah?

2-Muislamu anatumia facebook.Ikiwa facebook hiyo inatumika katika kheri na kwa ajili ya Allah pongezi kwako ewe ndugu yangu wa kiislamu. Je ikiwa facebook hiyo muislamu unaitumia katika dhambi nini utamjibu Allah (subhanahu wataala) baada ya kufikwa na mauti?

Malaika wa roho akija kukutoa roho huwa hakupi fursa ukafute picha za wanawake au wanaume ulizotumiana na wenzako. Hakupi fursa ukafute picha za uchi ulizopiga na kumtumia mwanamme au mwanamke. Hakupi fursa ukafute mazungumzo yako ya kimapenzi katika njia ya haramu. Hakupi fursa ukafute comment zako za matusi kwa watu. Hakupi fursa ukafute message zako za matusi ulizowatumia watu. Hakupi fursa ukafute yale uliyoyaweka katika kurasa yako na watu wanaona?

Je umeona uzito wake? Je kweli unalo jibu la kumjibu Allah (subhanahu wataala) ikiwa hali yako ni hiyo sasa? Malaika wa roho anarejesha roho kwa Allah inbox yako facebook imejaa picha na mazungumzo ya haramu. Facebook yako umeweka nyimbo na mambo mengine ya kuwafurahisha wanaadamu na kumkera mola wa walimwengu na ulimwengu. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Kwa hakika wale wanao penda uenee uchafu kwa walio amini, watapata adhabu chungu katika dunia na Akhera. Na Mwenyezi Mungu anajua na nyinyi hamjui.” (Suratu Nnuur:19).

3- Muislamu anatumia whatsapp. Ikiwa ni katika njia ya kheri basi Allah akuridhie. Je ikiwa ni kwa shari?
Muislamu husambaza nyimbo ndani ya whatsapp. Husambaza video za ngono na picha za ngono  iwe video hiyo kajirikodi yeye au picha hiyo kajipiga yeye au mwengine. Tena wengine husema wanaficha sura. Je unamficha mpaka Allah (subhanahu wataala) anaejua mpaka yaliyojificha ndani ya kifua chako?

Muislamu husambaza haramu yoyote ile na huku anacheka akiona anawafurahisha wenzake. Tena wako wanaosifiwa fulani kila siku hakosi jipya. Naam sifa za kidunia zimemlevya ila je anajua kuwa kila atakaengalia yale aliyotuma anapata dhambi? Je hajiulizi akifa leo watu wataangalia video zile au picha ile kwa miaka mingapi na ni wa ngapi wataangalia? Je anajua na yeye anapata dhambi kwani alichangia kusambaza uchafu? Allah (subhanhu wataala) anasema "Na hapana shaka wataibeba mizigo yao na mizigo mingine pamoja na mizigo yao. Na kwa yakini wataulizwa Siku ya Kiyama juu ya waliyo kuwa wakiyazua."(Suratul Ankabut:13).

  Wengine husambaza aibu za watu kwenye whatsapp,matusi na habari za uongo. Je malaika wa kutoa roho anakuja kuchukua amana ya roho. Nini atamjibu mola wa viumbe vyote?

Isituhadae dunia na vilivyomo ndani yake. Zisituhadae pumzi na kusahau akhera zetu. Tusifuate matamanio ya nafsi zetu. Tusije kujuta wakati huo wakati ambao majuto hayana tena faida. “Na watasema: Lau kuwa tungelisikia, au tungelikuwa na akili, tusingelikuwa katika watu wa Motoni!." Wakakiri dhambi zao. Basi kuangamia ni kwa watu wa Motoni!.” Suratul Mulk : 10-11)

Turudini kwa Allah (subhanahu wataala) na tukae katika njia yake. Hata yule ambae kishayafanya basi akitubia kwa Allah tawba ya kweli basi Allah atamsamehe. Allah (subhanahu wataala) anasema “Sema: Enyi waja wangu walio jidhulumu nafsi zao! Msikate tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu husamehe dhambi zote. Hakika Yeye ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu”.(Suratu Zumar : 53).
ALLAH TUJAALIE WALE WENYE KUAMBIWA MAZURI NA KUYAFANYIA KAZI NA KUKATAZWA MABAYA NA KUYAWACHA"Aaamin.

“Na iogopeni Siku ambayo mtarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, kisha kila nafsi italipwa ilicho chuma. Nao hawatadhulumiwa.”(Suratul Baqara:281).

Makala Imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group.

Friday 24 October 2014

UKUMBUSHO KWA WENYE KUFANYA MIJADALA NDANI YA MITANDAO YA KIJAMII NA KUISHIA MATUSI AU KUZUA NDANI YA DINI

Makala Imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah (subhanahu wa ta‘ala) Muumba wa kila kilichomo katika ulimwengu huu. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam).

Katika makala yangu ya leo nakusudia kupeleka nasaha zaidi kwangu binafsi pamoja na ndugu zangu wa kiislamu ambao hutumia mitandao ya kijamii kwa njia ya kujadiliana mambo mbali mbali ya kidini au ya kijamii.

Kumekuwa na maumivu makubwa ndani ya nafsi za waumini mbalimbali ambao huwa wanasoma maoni na mijadala ya dini ya waislamu ndani ya mitandao ya kijamii. Mijadala yenye hekima inafaa kwani inaleta funzo ndani ya jamii na kukosoana pale watu walipokosea. Ila mingi ya mijadala hiyo imekuwa haina heshima. Imekosa busara, na mwisho ni maneno machafu ambayo hata kuyaandika mfano wake siwezi. Leo nitajaribu kuyazungumza haya mambo kwa uchache ili tuweze kupeana tahadhari ili tusije kujuta siku ambayo mwanadamu hayatomfaa majuto yake. Miongoni mwa mambo yanayofanywa ni kama yafuatayo :

1-MATUSI YA NGUONI NA MANENO MACHAFU

Kwa hakika ukiwa unaangalia mijadala ndani ya facebook au whatsapp wengi wa watu huishia katika kutukanana na kutoleana maneno machafu. Ikiwa muislamu mwenzako hakubaliani na msimamo wako basi usimtukane wala usimwite majina mabaya au kumwambia maneno yasiyofaa. Tumia hekima katika kumfanya yule mtu aweze kukufahamu na aweze kukuelewa kile unachokikusudia. Lau angekuwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam),masahaba zake na wema wengine waliopita kazi yao kutukanana tu katika kufikisha daawa kweli uislamu ungekuwa na hali gani?

Daawa yao na mijadala yao ilikuwa ni daawa iliyojengwa na misingi ya Allah (subhanahu wataala) iliyotajwa ndani ya Quraan “Waite waelekee kwenye Njia ya Mola wako Mlezi kwa hikima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora. Hakika Mola wako Mlezi ndiye anaye mjua zaidi aliye ipotea Njia yake, na Yeye ndiye anaye wajua zaidi walio ongoka”(16:125)

Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) anaambiwa hata akijadiliana na wasiokuwa waislamu basi ajadiliane nao kwa namna iliyobora. Vipi baina ya muislamu kwa muislamu mwenzake? Vipi mazungumzo ya muislamu na muislamu mwenzake? Unadhani kuandika matusi na maneno yasiyofaa ndio utakuwa mtetezi wa uislamu? Hapana bali utakuwa ndio mpingaji wa aya za Quraan. Hebu tuangalie ndani ya Suratul Hujurati Allah ndani ya aya ya 11 Allah (subhanahu wataala) anasema “Wala msivunjiane hishima, wala msiitane kwa majina ya kejeli. Ni uovu kutumia jina baya baada ya kwisha amini.” Je haya yote waislamu tunayasahau?

Kumtukana muislamu mwenzako na asiyekuwa muislamu ni makosa ndani ya dini yetu. Tutumie lugha nzuri na laini baina yetu na baina ya wasiokuwa waislamu. Na yule ambae atakutukana basi wewe usirejeshe kwa tusi fahamu kuwa bado hajaijua haki siku akiiijua hatofanya hivyo.

Tuwe wapole na wenye kuheshimiana daima baina yetu.

2-KUZUSHWA KWA HADITHI ZA UONGO

Wakati watu wanapojadiliana wako watu huvuka mipaka na kuzusha yale yasiyokuwemo ndani ya dini. Wako wanaotunga hadithi na wako wengine wanaotoa fatwa kwa mambo wasiyokuwa na elimu nayo.

Ndugu zangu wa kiislamu tumuogopeni Allah (subhanahu wataala) tusitunge au tusiseme jambo ambalo halimo ndani ya Quraan wala sunna. Kama jambo hulijui ni bora kukaa kimya kuliko kuzua. Je unajua ni yapi yanayomsibu mwenye kuzua katika dini? Kutoka kwa Bibi Aisha(Radhiya Allahu anha) kuwa Mtume (Swalla Allahu alayhi wa aalihi wasallam) amesema : “Atakayezua akatia katika Dini yetu hii ambacho hakiko atarejeshewa mwenyewe.” (Al Bukhaariy na Muslim).

3-KUJITUKUZA KWA MTU KWA DHEHEBU LAKE AU ELIMU YAKE

Wako watu huwa wanajigamba na kujisifu kutokana na misimamo yake. Na huwa anaona ni rahisi sana kuwaambia waislamu wengine kuwa ni watu wa motoni na yeye na wenye kufuata madhehebu au misiamamo aliyokuwa nayo yeye ndio watu wa peponi na wako sahihi. Ni nani aliyekupa darja ya kuwaweka watu peponi na motoni? Ni nani aliyekwambia wengine uwadharau. Huo sio uislamu.

Tukhitalifiane lakini tusitoane kwenye uislamu wala tusiingizane motoni. Kwani hiyo ni kazi yake Allah (subhanahu wataala) peke yake. Bali sisi tukae kwa upendo nah uruma baina yetu. Allah (subhanahu wataala) anasema “Basi msijisifu usafi. Yeye anamjua sana mwenye kujikinga na maovu.”(53:32).

Wako wengine wao hujiona ndio wenye elim una ndio wana haki ya kusema kila kit una wasemalo wao ndio sahihi ya wengine si sahihi. Huku ni kukosa kwa elim una adabu zake. Na inampasa muislamu ajiepushe na tabia hizo. Kwani kujionesha na kibri kuna makatazo makubwa ndani ya uislamu. Imepokelewa kutoka kwa Abdullah bin Masud (Radhi za Allah ziwe juu yake) kwamba Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema:"Hatoingia Peponi ambaye moyoni mwake mna chembe ya kiburi". Mtu mmoja akauliza: “Mtu hupenda nguo yake iwe nzuri na viatu vyake viwe vizuri (itakuwaje?)” Akasema: "Hakika Allaah ni Mzuri Anapenda Uzuri. Kiburi ni kukataa haki na kudharau watu)"Muslim

Amesema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) :“Ninachokuogopeeni sana ni Shirki ndogo.)) Maswahaba wakauliza: "Ni nini hii Shirki ndogo, ewe Mtume wa Allah?" Mtume (Swalla Allahu alayhi waaalihi wasallam) akasema: Riya (kujionyesha).” [Imepokewa na Imaam Ahmad]

Nasaha zangu kwa waislamu tutumieni mitandao ya kijamii kwa uzuri. Daima tujue kuwa kila tunalolifanya linaandikwa na tutakuja kuyakuta katika kitabu chetu. Tuitumie mitandao hii kwa kujua kuwa Allah (subhanahu wataala) anatuona. Ikiwa binaadamu mwenzako unamuonea haya akuone ukiwa katika jambo ovu je huoni haya jicho la Allah likiwa linakuona unamuasi yeye na unafanya kinyume na alivyoamrisha?

Tutubieni kwa Allah (subhanahu wataala) toba ya kweli na tuache kabisa yale tuliyokuwa tunayafanya. Allah (subhanahu wataala) anasema “Hatamki neno ila karibu yake yupo mwangalizi tayari.”(50:19). Na anasema tena Allah (subhanahu wataala) “Leo tunaviziba vinywa vyao, na iseme nasi mikono yao, na itoe ushahidi miguu yao kwa waliyo kuwa wakiyachuma.”(36:65). Tukumbuke aya ya Allah (subhanahu wataala) isemayo ““Na iogopeni Siku ambayo mtarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, kisha kila nafsi italipwa ilicho chuma. Nao hawatadhulumiwa.”(2:281).

Thursday 23 October 2014

JINSI YA KUITUNZA NDOA YAKO

Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

BISMILLAHI RRAHMANI RRAHIM

Namshukuru Allah kwa kunipa nafasi hii ya kuandika makala adhimu kama hii ambayo endapo itafanyiwa kazi na Allah سبحانه وتعالىakaitilia Tawfiq basi itakua ni sababu ya kuleta manufaa makubwa katika jamii. Kisha swala na salam zimuendee kipenzi chetu Mtume Muhammad (sawﷺ).

Ama baada ya utangulizi huo sasa nitaingia rasmi katika uwanja mpana wa ndoa. Na leo nimependa kuzielekeza nasaha zangu zaidi kwa upande wa kina dada Ni jinsi gani watazilinda ndoa zao.

Kama tunavyofahamu ya kuwa ndoa ni mafungamano ya hiari baina ya mke na mume kuishi kwa pamoja kwa mapenzi na huruma mpaka mwisho wa maisha yao. Hivyo kwa kutambua hili inabidi kila mmoja wao awe ni mwenye pupa katika kuyafanya mambo ambayo yatakayozidisha mapenzi ya mwenza wake ili lipate kupatikana lengo kuu la ndoa ambalo ni utulivu wa nafsi.

Leo nimependa kuwabainishia mambo ambayo endapo mke atamfanyia mumewe basi yatazidisha mapenzi makubwa kwa mumewe kwani wengi wetu tunashindwa kuyafahamu ima kwa ufinyu wa fikra zetu au kwa sababu ni wapya katika ndoa.
Yafuatayo ndio mambo yakumfurahisha mumeo ili kuiimarisha ndoa yako:

1-KUWA MTIIFU KWAKE KATIKA MEMA ANAYOKUAMRISHA.

Tukizungumzia suala la utiifu ninamaanisha kuyatekeleza yale anayoyataka uyafanye katika yale yanayoridhiwa na Allah (subhanahu wataala). Kila binaadamu huwa ana mambo anayoyapenda afanyiwe na anayoyachukia yani hapendi afanyiwe. Na hali hii inatofautiana kutokana na mtu mmoja na mwengine. Kwa kua kuna mambo ambayo wengine kwao ni kawaida lakini kwa wengine huwa ni kero..Mfano Kumwita mumeo majina mazuri ya mapenzi kama mpenzi, laazizi, honey wapo wanaume ambao wanapenda na wanajihisi fahari kwa kuitwa majina haya na wake zao ima wakiwa peke yao au mbele za watu. Lakini wengine huwa hawapendi au wanapenda waitwe majina mazuri wakiwa faragha na wake zao au hupendelea kuitwa majina yao halisi. Katika hali hii inabidi mke uende na namna mumeo anavyopenda na sio kumwita kwa namna upendavyo wewe. Nadhani nitakua nimefahamika katika hili.

Na Kumtii mume ni katika ibada takatifu sana ambazo humpeleka mwanamke peponi atakapoifanya na kumuingiza motoni atakapoenda kinyume nayo. Amesema Mtume(ﷺ) “Atakapo swali mwanamke swala zake tano(za faradhi), akafunga mwezi wake (wa ramadhani), akajihifadhi utupu wake (kwa stara inayotakikana na hakutoka nje ya ndoa yake), na akamtii mumewe ataambiwa siku ya kiama INGIA PEPONI KWA MLANGO UUPENDAO” Imepokelewa na Imam Ahmad.

Pia suala la kumtii mume ni katika ishara za imani. Kwani Allah Subhanahu wataala amesema katika Qur'an tukufu :((Enyi mlio amini! Mtiini Mwenyezi Mungu, na mt'iini Mtume na wenye madaraka katika nyinyi...))(4:59) .Na katika wenye madaraka juu yetu sisi wanawake ni waume zetu ambao wamekubali kuchukua dhima kutoka kwa wazazi wetu. Hivyo ili kuipata imani ya kisawa sawa inabidi tuwe watiifu kwa Allah, Mtume na Waume zetu bila ya kuwasahau wazazi wetu kwani nao bado wanahaki na sisi. Allah atuwafikishe katika hili.

2-Ridhika na Alichonacho

Katika mambo ambayo huongeza mapenzi mno katika ndoa ni wanandoa kutosheka. Namaanisha kwamba kila mmoja awe ameridhika na hali yoyote atakayomkuta nayo mwenzake. Na hawi na sifa hii ila yule mwenye mapenzi ya dhati kwa mwenzake na pia mwenye imani katika kifua chake kwani hakika muumini siku zote hutosheka na alichonacho na kuridhia kwamba ni qadar ya Allah (subhanahu wataala) aliyomkadiria. Amesema Mtume (ﷺ) : (( Ridhia katika kile alichokugawia Allah utakua ni tajiri zaidi kuliko watu)) Attirmidhiy.

Na pia katika hadithi nyengine amesema Mtume (ﷺ) “Hakika amefaulu aliesilimu na akaruzukiwa kinachomtosheleza na akakinaishwa na Allah kwa kile alichomruzuku”. Muslim.
Hadithi hizi mbili zinatufundisha tuwe wenye kukinai na kile tulichoruzukiwa kwani ni sababu ya kufaulu hapa duniani mpaka kesho akhera.

3-MTUNZIE SIRI ZAKE

Hakika katika mambo yanayochukiza mbele ya Allah (subhanahu wataala) na yatakayomsababishia mtu kupata adhabu kali ni mke au mume kutoa siri za mwenzake kwa nia mbaya yaani kumfedhehesha. Kwani amesema Mtume (ﷺ) katika kuelezea hili: ((Hakika katika watu wenye nafasi mbaya siku ya Qiyaamah ni mwanaume anaemuendea mkewe au mke anaeendewa na mumewe (wakafanya tendo la ndoa) halafu akaeneza siri ile)). Muslim. Hadithi hii imemkemea kila mwanaume na mwanamke mwenye kueneza siri za mwenzake.

Hivyo ni wajibu wetu kuwa makini na hili kwani tutakapojiepusha nalo tutakuwa miongoni mwa wanawake wema.

4-MUAMINI MUMEO

Uaminifu baina ya wanandoa ni jambo muhimu sana linalopelekea ndoa kuwa madhubuti ama kinyume na hapo ndoa hulega lega na kupelekea kuvunjika. Katika suala la uaminifu kila mmoja anatakiwa kuwa ni muaminifu kwa mwenzake sawa sawa wapo karibu au mbali mbali.

Muamini mumeo na wala usimtilie mashaka kwani kumtilia mashaka kutakuondolea mapenzi katika moyo yako. Na pia usichukue hatua yoyote kwa jambo la kuambiwa haswa litakapotoka kwa mtu ambae anajulikana kwa tabia zake kuwa ni mfitinishaji na ni mchochezi baina ya ya watu. Kwani hata Allah Subhanahu Wataala ametuambia ndani ya Qur'an : ((Enyi mlio amini! Akikujieni mpotovu na khabari yoyote, ichunguzeni, msije mkawasibu watu kwa kuto jua, na mkawa tena wenye kujuta kwa mliyo yatenda.)) 49: 6

Hivyo utakaposikia jambo lolote baya kuhusu mumeo ni bora kulihakikisha mwenyewe kwa macho au masikio yako ili usije ukaharibu ndoa yako kwa sababu zisizo na msingi.

5-JIPENDEZESHE KW AJILI YAKE

Tambua ewe dada wa kiislamu kwamba kujipamba kwa ajili ya mume wako ni ibada na utalipwa kupitia ibada hio. Utakapopenda kujipendezesha kwa ajili ya mumeo kwa namna mbali mbali zilizo za kheri (zinazoruhusiwa na sheria) basi mumeo hatakuchoka na kinyume chake atatamani kila anapopata fursa akimbilie ndani kwake kwani wewe mkewe ni sababu ya tulizo la macho yake na moyo wake.

Kinyume na hapo mke ukiwa hujipambi kwa ajili ya mumeo kwanza unapata madhambi kwa sababu wewe ndio unakua chanzo cha yeye kutafuta tulizo la jicho na moyo wake katika vilivyo vya haramu. Pili wewe kama utakua unajipamba nje ya nyumba yako basi nawe utakua unapata madhambi kwani Allah(subhanahu wataala) ametukataza kuyabainisha mapambo yetu ila kwa wale wasioruhusiwa kutuoa yani baba, kaka, mjomba, babu, baba mkubwa au mdogo na watu wanaokuhusu kwa damu au ulionyonya nao.

Allah(subhanahu wataala) anatuambia: ((Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao isipokuwa unao dhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao, au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au kaka zao, au wana wa kaka zao, au wana wa dada zao, au wanawake wenzao, au iliyo wamiliki mikono yao ya kuume, au wafwasi wanaume wasio na matamanio, au watoto ambao hawajajua mambo yaliyo khusu uke. Wala wasipige chini miguu yao ili yajuulikane mapambo waliyo yaficha. Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa.))24:31

Aya hii nadhani haihitaji ufafanuzi kwani yenyewe ilivyo imejitosheleza. Na ametukuka Allah kwani hatuamrishi ila lililo na kheri nasi na hatukatazi ila lililo na madhara nasi duniani mpaka kesho akhera.