Thursday 23 October 2014

JINSI YA KUITUNZA NDOA YAKO

Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

BISMILLAHI RRAHMANI RRAHIM

Namshukuru Allah kwa kunipa nafasi hii ya kuandika makala adhimu kama hii ambayo endapo itafanyiwa kazi na Allah سبحانه وتعالىakaitilia Tawfiq basi itakua ni sababu ya kuleta manufaa makubwa katika jamii. Kisha swala na salam zimuendee kipenzi chetu Mtume Muhammad (sawﷺ).

Ama baada ya utangulizi huo sasa nitaingia rasmi katika uwanja mpana wa ndoa. Na leo nimependa kuzielekeza nasaha zangu zaidi kwa upande wa kina dada Ni jinsi gani watazilinda ndoa zao.

Kama tunavyofahamu ya kuwa ndoa ni mafungamano ya hiari baina ya mke na mume kuishi kwa pamoja kwa mapenzi na huruma mpaka mwisho wa maisha yao. Hivyo kwa kutambua hili inabidi kila mmoja wao awe ni mwenye pupa katika kuyafanya mambo ambayo yatakayozidisha mapenzi ya mwenza wake ili lipate kupatikana lengo kuu la ndoa ambalo ni utulivu wa nafsi.

Leo nimependa kuwabainishia mambo ambayo endapo mke atamfanyia mumewe basi yatazidisha mapenzi makubwa kwa mumewe kwani wengi wetu tunashindwa kuyafahamu ima kwa ufinyu wa fikra zetu au kwa sababu ni wapya katika ndoa.
Yafuatayo ndio mambo yakumfurahisha mumeo ili kuiimarisha ndoa yako:

1-KUWA MTIIFU KWAKE KATIKA MEMA ANAYOKUAMRISHA.

Tukizungumzia suala la utiifu ninamaanisha kuyatekeleza yale anayoyataka uyafanye katika yale yanayoridhiwa na Allah (subhanahu wataala). Kila binaadamu huwa ana mambo anayoyapenda afanyiwe na anayoyachukia yani hapendi afanyiwe. Na hali hii inatofautiana kutokana na mtu mmoja na mwengine. Kwa kua kuna mambo ambayo wengine kwao ni kawaida lakini kwa wengine huwa ni kero..Mfano Kumwita mumeo majina mazuri ya mapenzi kama mpenzi, laazizi, honey wapo wanaume ambao wanapenda na wanajihisi fahari kwa kuitwa majina haya na wake zao ima wakiwa peke yao au mbele za watu. Lakini wengine huwa hawapendi au wanapenda waitwe majina mazuri wakiwa faragha na wake zao au hupendelea kuitwa majina yao halisi. Katika hali hii inabidi mke uende na namna mumeo anavyopenda na sio kumwita kwa namna upendavyo wewe. Nadhani nitakua nimefahamika katika hili.

Na Kumtii mume ni katika ibada takatifu sana ambazo humpeleka mwanamke peponi atakapoifanya na kumuingiza motoni atakapoenda kinyume nayo. Amesema Mtume(ﷺ) “Atakapo swali mwanamke swala zake tano(za faradhi), akafunga mwezi wake (wa ramadhani), akajihifadhi utupu wake (kwa stara inayotakikana na hakutoka nje ya ndoa yake), na akamtii mumewe ataambiwa siku ya kiama INGIA PEPONI KWA MLANGO UUPENDAO” Imepokelewa na Imam Ahmad.

Pia suala la kumtii mume ni katika ishara za imani. Kwani Allah Subhanahu wataala amesema katika Qur'an tukufu :((Enyi mlio amini! Mtiini Mwenyezi Mungu, na mt'iini Mtume na wenye madaraka katika nyinyi...))(4:59) .Na katika wenye madaraka juu yetu sisi wanawake ni waume zetu ambao wamekubali kuchukua dhima kutoka kwa wazazi wetu. Hivyo ili kuipata imani ya kisawa sawa inabidi tuwe watiifu kwa Allah, Mtume na Waume zetu bila ya kuwasahau wazazi wetu kwani nao bado wanahaki na sisi. Allah atuwafikishe katika hili.

2-Ridhika na Alichonacho

Katika mambo ambayo huongeza mapenzi mno katika ndoa ni wanandoa kutosheka. Namaanisha kwamba kila mmoja awe ameridhika na hali yoyote atakayomkuta nayo mwenzake. Na hawi na sifa hii ila yule mwenye mapenzi ya dhati kwa mwenzake na pia mwenye imani katika kifua chake kwani hakika muumini siku zote hutosheka na alichonacho na kuridhia kwamba ni qadar ya Allah (subhanahu wataala) aliyomkadiria. Amesema Mtume (ﷺ) : (( Ridhia katika kile alichokugawia Allah utakua ni tajiri zaidi kuliko watu)) Attirmidhiy.

Na pia katika hadithi nyengine amesema Mtume (ﷺ) “Hakika amefaulu aliesilimu na akaruzukiwa kinachomtosheleza na akakinaishwa na Allah kwa kile alichomruzuku”. Muslim.
Hadithi hizi mbili zinatufundisha tuwe wenye kukinai na kile tulichoruzukiwa kwani ni sababu ya kufaulu hapa duniani mpaka kesho akhera.

3-MTUNZIE SIRI ZAKE

Hakika katika mambo yanayochukiza mbele ya Allah (subhanahu wataala) na yatakayomsababishia mtu kupata adhabu kali ni mke au mume kutoa siri za mwenzake kwa nia mbaya yaani kumfedhehesha. Kwani amesema Mtume (ﷺ) katika kuelezea hili: ((Hakika katika watu wenye nafasi mbaya siku ya Qiyaamah ni mwanaume anaemuendea mkewe au mke anaeendewa na mumewe (wakafanya tendo la ndoa) halafu akaeneza siri ile)). Muslim. Hadithi hii imemkemea kila mwanaume na mwanamke mwenye kueneza siri za mwenzake.

Hivyo ni wajibu wetu kuwa makini na hili kwani tutakapojiepusha nalo tutakuwa miongoni mwa wanawake wema.

4-MUAMINI MUMEO

Uaminifu baina ya wanandoa ni jambo muhimu sana linalopelekea ndoa kuwa madhubuti ama kinyume na hapo ndoa hulega lega na kupelekea kuvunjika. Katika suala la uaminifu kila mmoja anatakiwa kuwa ni muaminifu kwa mwenzake sawa sawa wapo karibu au mbali mbali.

Muamini mumeo na wala usimtilie mashaka kwani kumtilia mashaka kutakuondolea mapenzi katika moyo yako. Na pia usichukue hatua yoyote kwa jambo la kuambiwa haswa litakapotoka kwa mtu ambae anajulikana kwa tabia zake kuwa ni mfitinishaji na ni mchochezi baina ya ya watu. Kwani hata Allah Subhanahu Wataala ametuambia ndani ya Qur'an : ((Enyi mlio amini! Akikujieni mpotovu na khabari yoyote, ichunguzeni, msije mkawasibu watu kwa kuto jua, na mkawa tena wenye kujuta kwa mliyo yatenda.)) 49: 6

Hivyo utakaposikia jambo lolote baya kuhusu mumeo ni bora kulihakikisha mwenyewe kwa macho au masikio yako ili usije ukaharibu ndoa yako kwa sababu zisizo na msingi.

5-JIPENDEZESHE KW AJILI YAKE

Tambua ewe dada wa kiislamu kwamba kujipamba kwa ajili ya mume wako ni ibada na utalipwa kupitia ibada hio. Utakapopenda kujipendezesha kwa ajili ya mumeo kwa namna mbali mbali zilizo za kheri (zinazoruhusiwa na sheria) basi mumeo hatakuchoka na kinyume chake atatamani kila anapopata fursa akimbilie ndani kwake kwani wewe mkewe ni sababu ya tulizo la macho yake na moyo wake.

Kinyume na hapo mke ukiwa hujipambi kwa ajili ya mumeo kwanza unapata madhambi kwa sababu wewe ndio unakua chanzo cha yeye kutafuta tulizo la jicho na moyo wake katika vilivyo vya haramu. Pili wewe kama utakua unajipamba nje ya nyumba yako basi nawe utakua unapata madhambi kwani Allah(subhanahu wataala) ametukataza kuyabainisha mapambo yetu ila kwa wale wasioruhusiwa kutuoa yani baba, kaka, mjomba, babu, baba mkubwa au mdogo na watu wanaokuhusu kwa damu au ulionyonya nao.

Allah(subhanahu wataala) anatuambia: ((Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao isipokuwa unao dhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao, au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au kaka zao, au wana wa kaka zao, au wana wa dada zao, au wanawake wenzao, au iliyo wamiliki mikono yao ya kuume, au wafwasi wanaume wasio na matamanio, au watoto ambao hawajajua mambo yaliyo khusu uke. Wala wasipige chini miguu yao ili yajuulikane mapambo waliyo yaficha. Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa.))24:31

Aya hii nadhani haihitaji ufafanuzi kwani yenyewe ilivyo imejitosheleza. Na ametukuka Allah kwani hatuamrishi ila lililo na kheri nasi na hatukatazi ila lililo na madhara nasi duniani mpaka kesho akhera.

1 comment: