Saturday 18 October 2014

SIMU ZA MIKONONI NA NDOA ZETU

Makala hii Imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group.

Kila sifa njema zinamstahikia Allah (subhanahu wa ta‘ala) Muumba wa kila kilichomo katika ulimwengu huu. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam).

Kwa hakika katika elimu aliyowajaalia Allah (subhanahu wataala) waja wake ni uvumbuzi wa mambo mbalimbali. Katika yaliyovumbuliwa mengine huwa na faida na mengine huwa na hasara. Simu ya mkononi ni miongoni mwa kifaa kilichovumbuliwa. Simu ina faida zake ikiwemo kurahisisha mawasiliwano baina ya mtu na mtu mwengine,kuweka ukaribu kwa familia au marafiki. Lakini kwa hakika kwa sasa simu ina madhara makubwa sana kwetu sisi. Na ni wachache sana ambao wamesalimika na fitna hizi au madhara yake.

Leo katika makala hii nakusuduia kuzungumzia jinsi simu za mikononi zinavyoharibu ndoa zetu na hata kupelekea kuvunjika kwa ndoa hizo. Ziko ndoa nyingi sana zimekwisha kwa wanawake kupewa talaka au kwa kuomba talaka na sababu kubwa simu za mikononi. Namuomba Allah ajaalie tawfiq iwe ni sababu kwa kila atakaesoma makala hii ya kujirekebisha pale alipokosea.

1-MAZUNGUMZO YA KIMAPENZI BAINA YA MWANANDOA NA MTU AMBAE SIO MWANANDOA MWENZAKE

Ni simu ngapi ndani yake zimekutwa na ujumbe wa kimapenzi. Ujumbe ambao mtu hajatumiwa na mke wake au mume wake. Tena huwa ni ujumbe wa mapenzi unaoshiria kuwa mke au mume ni mwenye kutoka nje ya ndoa yake. Linapotokea jambo hilo kwa wanandoa wako wengine hujifanya mafundi wa kusema uongo na wengine huishia kutoa maneno na kukosa jibu. Au mwanamme kujifanya yeye ndio bwana hatakiwi kuhojiwa. Na hata wengine huishia kupiga wake zao kwa sababu tu ya kushika simu yake.

Kwa nini mtu ukose uaminifu kwa mwanandoa mwenzako? Kwa nini utumiwe ujumbe wa kimapenzi na mtu asiyekuwa mume wako au mke wako? Hivi unadhani hesabu yako hutaikuta kwa Allah? Kwa nini simu imekuwa inawekwa password ambayo haambiwi mke ikiwa na mume au haambiwi mume ikiwa ni mke? Tunakwenda wapi enyi umma wa kiislamu? Kwa nini tunazifisidi ndoa zetu kwa kufuata matamanio ya nafsi zetu?

Napenda kutoa nasaha kwa wanandoa unapokuta ujumbe ambao unaashiria machafu kwa mume wako au mke wako basi usikimbilie kutoa maneno au kufanya yasiyostahiki. Kwanza uliza kwa hekima na uwe na subra yawezekana ni fitna tu imeundwa ili kukuharibieni ndoa zenu. Na haya yapo na tayari yameshavunja ndoa za watu kumbe ni jambo lililopangwa na kuzuliwa. Kwani Allah (subhanahu wataala) anasema “Enyi mlio amini! Akikujieni mpotovu na khabari yoyote, ichunguzeni, msije mkawasibu watu kwa kuto jua, na mkawa tena wenye kujuta kwa mliyo yatenda.”(49:6). Ndio chunguza kwanza ili baadae usije kujuta kwa kumuingiza mwenzako kwenye makosa yasiyokuwa yake.

Na ewe uliyeoa au kuolewa acha tabia za kutoka nje ya ndoa yako. Umeaminiwa basi na wewe jiaminishe. Kwani hakika ni alama ya unafik yule anaeaminiwa akavunja uaminifu wake. Tambua kuwa Allah (subhanahu wataala) anakuona na tambua hakuna la siri kwake na ipo siku siri hiyo itatoka tena itakuwa ni siku ya majuto makubwa na fedheha. Na mwisho wake kuingia katika moto. Allah atuhifadhi. Allah (subhanahu wataala) anasema “Siku zitakapo dhihirishwa siri.”(86:9).

2-KUKUTWA NA PICHA ZISIZOKUWA NA HESHIMA NDANI YA SIMU

Siku hizi kuna whatsapp na facebook hizi nazo zina mchango mkubwa sana kuharibu ndoa zetu. Mwanamme anakuwa na picha za wanawake wakiwa hawana mavazi au mwanamke nae kukutwa na picha za wanaume. Je unadhani ni lipi ambalo mume wako au mke wako ataweza kulifahamu akikutana na hali hizo?

Picha kama hizi zinapatikana kwa aina mbili kuu kwanza ni picha zinazoezwa kwenye mitandao ya kijamii na watu ambao hawana khofu juu ya Allah na ni wenye kumuasi Allah (subhanahu wataala). Na pili huwa ni picha ambazo mwanamke au mwanamme ameziomba kwa watu wao ambao hufanya mambo ya haramu.

Umeoa au umeolewa kwa lengo upate utulivu wa nafsi. Na ukapewa uhuru uoe katika uwapendao na uolewe na yule umpendae. Sasa hili suala la kutafuta picha zisizokuwa na maana ten aza haramu zinatoka wapi?

Tena wanandoa wengine wanakutwa na picha hizo wakiwa na wanaume zao au wanawake zao ambao wanafanya nao maasi hali ya kuwa na wao wameolewa au wameoa? Ni wanawake wangapi au wanaume wangapi tayari wameshakutwa na kesi ya kukutwa na picha za wanaume au wanawake ambao sio jamaa zake ziwe za heshima au sio za heshima? Lazima mke au mume ataumia kwa sababu ya wivu. Haya yote yanasababishwa na simu zetu za mikononi. Tujiepusheni na tabia hii ili kuzilinda ndoa zetu.

3-KUJIFICHA NA SIMU WAKATI WA MAZUNGUMZO

Wengi wa wanandoa wenye kutoka nje ya ndoa zao huwa wanaogopa kuzungumza na simu mbele ya wake zao. Na ikiwa anazungumza huwa anajifanya huyo mtu hamjui kabisa au huwa anababika katika mazungumzo. Na wako wengine hasa wanaume wanapoingia kwenye nyumba zao huzima simu sababu kubwa husema hataki kukerwa ila ni wachache wenye ukweli. Wengi wao hukimbia kutumiwa ujumbe na wanawake au kupigiwa simu na wanawake wa haramu. Kwa nini simu ikiwa kwako tu ndio inazimwa? Basi itoe sauti iweke pembeni.

Itunze ndoa yako. Usiweke mazingira ya mwenzako kukutilia shaka na itakuja kupelekea kuondosha uaminifu kwenye ndoa yenu.

Kwa hakika mada hii ni refu na ina mifano mingi sana. Naomba niishie hapa na nitoe nasaha zifuatazo : Simu zetu zisituhadae hadi tukawa tayari kuvunja ndoa zetu na zikatupeleka pabaya siku ya Qiyama. Tumuogopeni Allah (subhanahu wataala). Hebu kaa na utafakari ni pesa ngapi umehonga kwa wanawake au umetumia kwa ajili ya wanawake wakati mke wako wa halali unae ndani nae ana shida zake nyingi sana? Tambua unatumia neema za Allah na utakuja kuulizwa juu ya neema hizo. Ewe mwanamke itunze ndoa yako na usikubali kuipoteza ndoa yako kwa kukosa uaminifu. Dunia ni hadaa na hesabu zetu zote tutazikuta kwa Allah. Tukumbuke aya ya Allah (subhanahu wataala) isemayo ““Na iogopeni Siku ambayo mtarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, kisha kila nafsi italipwa ilicho chuma. Nao hawatadhulumiwa.”(2:281).

No comments:

Post a Comment